Sunday 15 September 2013

MSANII WA KWANZA KUREKODI KANDA ZA VICHEKESHO NCHINI


Mchekeshaji na mwigizaji nguli nchini, Amri Athumani maarufu King Majuto 


Majuto anasema kuwa baada ya kutoka Kenya alirejea nchini mwaka 1987 na kujiunga na Kundi la DDC Kibisa. Hata hivyo hakudumu muda mrefu na kundi hilo kwani aliugua Kifua Kikuu na kulazimika kukaa nje ya ulingo kwa mwaka mzima. Kabla ya kurejea alijiunga na Kundi la Muungano Cultural Troupe, alikwenda Kundi la Makutano.
Anasimulia kuwa alipoondoka Makutano alijiunga na Kundi la Super Mama lililokuwa na makazi yake Morogoro kabla ya kujiunga na Kundi la TOT mwaka 1993, lakini mwaka 1994 alijitoa kwenye kundi hilo baada ya kuona maslahi madogo.
Kuanzia hapo Majuto alianza kujitegemea kufanya kazi binafsi na kupata mikataba kwa watu na kampuni mbalimbali.
Anakumbuka Redio ya Abood ya mjini Morogoro kuwa ndiyo ilikuwa ya kwanza kumpa mkataba uliokuwa wa mwaka mmoja, ambapo alicheza mara moja kwa wiki na kila alipocheza alilipwa Sh200,000 na kutumia vifaa vya ofisi hiyo.

“Kazi hii ilinilipa sana, kwani hata bati nilizoezekea nyumba yangu nilizinunua huko. Abood ilinilipa vizuri na nilishirikisha familia kwa kipato changu. Mke wangu na wanangu walikuwa wakiigiza pamoja nami, hivyo kila kilichopatikana mimi ndiyo nilikuwa nakipangia matumizi na yalikuwa ya kifamilia,”anasema Majuto.
Kuanza kurekodi kanda za vichekesho
Anabainisha kuwa mwaka 1999 aliamua kurudi nyumbani kwao mkoani Tanga na kuanza kufanya maonyesho yake kwenye kumbi mbalimbali, ambapo alikutana na mtu aliyemtaja kwa jina moja la Ramjuuni (marehemu kwa sasa) na huyo ndiye aliyeanza kurekodi na kutoa mikanda ya vichekesho vya Majuto.
“Nilikuwa mtu wa kwanza kutoa vichekesho katika mikanda na ilikuwa ni analojia, haikuwa katika ubora unaotakiwa, lakini ndiyo nilizidi kuwa maarufu kupitia mikanda hii,”anasema Majuto.
Anasema kuwa nyingine iliyomfanya afahamike zaidi ni Vitimbi Mitaani, ambayo ilifanya kila mtu afahamu uwezo wake.
Kitu ambacho sintokisahau
Anasema kuwa baada ya kufanya kazi na watu wengi, aliingia mkataba na Kampuni ya Al- Riyami, iliyo chini ya Abdallah Riyami wenye thamani ya Sh20 milioni, bahati mbaya alipata ugonjwa wa na kulazimika kufanyiwa upasuaji.
Anabainisha kuwa baada ya kupona aliambiwa akae mwezi mmoja bila kufanya kazi, lakini bosi wake alimweleza kuwa akikaa muda huo bila kufanya kazi, hatomlipa kwa kuwa amemwajiri ili afanye kazi ndipo amlipe.
Anakumbuka kuwa pamoja na maneno hayo yeye alikuwa akidai Sh500,000 kwa bosi wake huyo, lakini alipokumbusha aliambiwa kuwa hatamlipa pesa hizo kwa kuwa Al- Riyami alikuwa akiwadai watoto wa Majuto waliokuwa wakifanya kazi dukani, aliodai walimtia hasara, hivyo Majuto akabaki hana kitu.
“Nikawa na njaa, huku nikiwa na familia. Nikaanza kucheza nje ya mkataba, Al- Riyami akachukia na kutaka kunipeleka mahakamani. Lakini, Mungu si Athumani, nikapata mtu wa kuokoa jahazi,”anasema Majuto huku akiangua kicheko.
Anasema kuwa hata hivyo, kabla ya kupelekwa mahakamani kwa mara ya kwanza akitakiwa kulipa kiasi hicho cha fedha za mkataba, Kampuni ya Azam Tv wakamwita kwa ajili ya kufanya naye kazi.
Anaweka wazi kuwa aliwaambia kuwa ana mkataba wa Al-Riyami ulio na deni analotakiwa kulipa na Azam wakalipa deni na kumchukua kwa mkataba mpya wa mwaka mmoja.
Chini ya mkataba huo Majuto ana uwezo wa kufanya kazi sehemu yoyote kwa masharti ya kutoa taarifa ili Azam wakimhitaji wampate.
Anaongeza kuwa alipata mkataba mnono wa Sh1 milioni papo hapo kila anaporekodi tangazo akipata pia mshahara wa Sh200,000 kwa mwezi akiwezeshwa pia kwa bidhaa zinazozalishwa na Kampuni ya Azam.
“Nagonga matangazo kwa ajili ya vipindi vya Tv Azam vitakavyoanza kurushwa hivi karibuni. Huwezi kuamini jinsi maisha yanavyobadilika uzeeni na ghafla,”anasema Majuto akifurahia, huku akitingisha mguu.
Biashara
Mbali na uigizaji, Majuto anafanya biashara ya usafirishaji abiria ndani ya Jiji la Tanga hutumia magari matatu anayomiliki maarufu kwa jina la King Majuto The Super Star.
Hata hivyo anasema haikuwa rahisi kumiliki biashara hiyo ambayo imetokana na uigizaji, kwani ilimbidi kupanga na kujua afanye nini kwanza kabla ya kuamua kufanya biashara hiyo, huku akilalamika kuwa hailipi kwa mji wa Tanga, tofauti na ilivyo kwa Dar es Salaam.
“Lakini kwa kuwa ameamua kuishi Tanga, nakubali matokeo. Hapo nyuma muda wa kukaa na familia yangu ulikuwa mdogo sana na nilikuwa nakimbizana na maisha, lakini sasa nina angalau ka uwezo kidogo waje wanaifuate wenyewe huku,”anasema Majuto.
Pamoja na daladala hizo Majuto pia anamiliki gari aina ya Noah ambalo ndiyo gari lake la kutembelea, hata anapofanya safari zake za kikazi.
Kwa nini aliamua kucheza filamu za kawaida.
Anasema kuwa kujiamini kuwa anaweza na kutaka kubadilika kulingana na kipaji chake ndivyo vilivyomsukuma kuanza kucheza filamu za kawaida.
“Njaa inakupa akili ya kufanya kitu tofauti ili kuongeza kipato na ndiyo hiyo hiyo inanifanya nibadilike kama kinyonga. Komedi mimi, filamu mimi, majukwaani mimi na bado hata ikija aina gani ya uigizaji, naamini nitaweza kwa kuwa hiki ni kipaji cha kuzaliwa nacho,”anasema Majuto.
Anaongeza kuwa mbali na njaa, katika tasnia ya filamu kuna umuhimu wa kuwepo watu kama yeye, ambao watakuwa ni kama washauri pale watakapoona kuna kitu kimekosewa.
Endelea kufuatilia sehemu ijayo ya makala kuhusu nguli King Majuto. Je, ataeleza nini kuhusu familia yake? Mama Majuto anasemaje.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...