Wednesday 13 November 2013

Dk. Mwakyembe aibukia bandari ya Tanga


Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe


Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, ametangaza rasmi kumalizika kwa fungate kwa watendaji wa serikali mkoani Tanga ikiwamo Mamlaka ya Bandari (TPA), Mamlaka ya Mapato (TRA) na Jeshi la Polisi, kutokana na kuhusika moja kwa moja na mtandao wa magendo hasa upitishaji wa dawa za kulevya na pembe za ndovu.

Hatua hiyo inafuatia kuwepo kwa bandari bubu 49 mkoani Tanga ambazo zimekuwa zikihusika na upitishaji wa bidhaa kwa  magendo ili kukwepa kodi, zikiwamo dawa za kulevya, wahamajia haramu na pembe za ndovu.

Dk. Mwakyembe aliyasema hayo jana wakati akizungumza na watendaji wa TPA, TRA, wafanyabiashara na wadau wanaotumia bandari ya Tanga muda mfupi tu baada ya ziara ya ukaguzi katika wilaya ya Pangani na bandari ya Tanga.

Alisema ili kuthibitisha kauli yake hiyo atawataja kwa majina wahusika na vinara wa mtandao huo na kwamba kuanzia sasa anatangaza rasmi vita baina yao.

“Tunawajua kwa majina msione tumekaa kimya tu na mitandao yenu tunaijua…jeshi la Polisi wanasaidia kuwasindikiza, yaani Tanga imekuwa ni kituo cha kupokea bidhaa haramu…sasa honeymoon (fungate), ndugu zangu imekwisha,” alisisitiza Waziri huyo.

Dk. Mwakyembe alieleza kutoridhishwa kwake na utendaji kazi wa TRA mkoani hapa na kusema kuwa ataliwakilisha kwa Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa ili hatua za haraka zichukuliwe.

Awali, akizungumza katika mkutano huo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Kipande Madeni, aliwataka watendaji wa mamlaka hiyo mkoa wa Tanga kuendela kujituma katika utekelezaji wao ikiwamo kufanya kazi kwa saa 24 kama wanavyofanya Dar es Salaam.

Naye Kaimu Meneja wa TPA Mkoa wa Tanga, Freddy Liundi, alisema kuwa bandari hiyo inatarajia kupokea vifaa aina ya Baji vyenye uwezo wa kupakua mzigo hadi wa tani 3,500 kwa kontena 196 zenye urefu wa futi 20 mwezi Disemba, mwaka huu.
 
SOURCE: NIPASHE     

No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...