Saturday 22 February 2014

NYONGEZA YA POSHO:JAJI AUGUSTINO ATEMA CHECHE

Jaji Mkuu Mstaafu,Augustino Ramadhani.

Hakuna kiasi cha fedha kinachopaswa kulipwa kwa yeyote anayefanya kazi ya kulitumikia taifa
  Kila mjumbe atangulize kwanza maslahi ya nchi

Jaji  Mkuu Mstaafu Augustino Ramadhani , amewataka  wajumbe wa Bunge la Katiba kutambua kuwa hakuna kiasi cha fedha kinachopaswa kulipwa kwa yeyote anayefanyakazi ya kulitumikia taifa.

Aliongeza kuwa ni vyema kabla ya kuomba nyongeza ya posho wakalikubali  suala hilo kuwa malipo kwa kazi ya utaifa hayana kiwango.

Jaji  Mkuu mstaafu, aliyasema hayo jana jijini  Arusha, wakati akifungua mkutano wa  mwaka wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), unaojadili mchakato wa mabadiliko ya katiba mpya.

Alitolea mfano kwa wanajeshi ambao wanakwenda vitani kupigana vita na baadhi wanapoteza maisha , lakini pamoja na fedha wanayopewa bado haiwezi kulinganishwa na uhai wa maisha yao uliopotea vitani.

Anazungumza hoja hiyo, wakati Bunge Maalumu la Katiba limeunda kamati ya kuangalia uwezekano wa kuongeza zaidi posho ya  wajumbe kwa siku kwa maelezo kuwa kiasi cha Sh. 300,000 wanachopewa  ni kidogo.

"Lakini Watanzania wengi hawalipwi Sh. 300,000 kwa siku, hivyo kinachotakiwa hapo  ni kwa kila mjumbe kutanguliza nchi kwanza,"alisema.

Aliongeza kuwa endapo wajumbe hao wataweka mbele  maslahi ya taifa, kazi iliyo mbele yao itakuwa rahisi na pia italeta manufaa kwa  vizazi vya sasa na  vijavyo.

Alisisitiza tena kuwa mawazo yaliyotolewa kwenye rasimu si ya mtu bali ni maoni ya wananchi hivyo hayawezi kubadilishwa na bunge hilo ambalo lina mipaka.

"Sisi Tume ya Mabadiliko tulifanya kazi kwa kuachana na uchama na kila aina ya kuonyesha maslahi ya mtu au kikundi fulani bali tulizingatia maoni ya wananchi,"alisema.

Kadhalika aliwakumbusha wajumbe wa Bunge la Katiba kusoma kifungu namba  25 cha sheria ya mabadiliko ya katiba ili wayafahamu mambo wanayoruhusiwa  na yale ambayo sheria inawazuia kuyazungumzia .

Katika mkutano huo, alisisitiza tena umuhimu wa kuzingatia maoni ya Watanzania na siyo kutanguliza maslahi ya vyama au ya watu binafsi. Alisema jukumu la wajumbe wa bunge hilo ni kuongeza mambo yaliyopungua na siyo kubadilisha misingi iliyopo ambayo imetolewa na wananchi wakati wa kukusanya maoni ya mabadiliko ya katiba.

"Mimi nawashauri wasome vizuri kifungu cha 25 cha sheria ya mabadiliko ya katiba, waone kama  anaruhusiwa au mambo gani wanapaswa kuyafanya,"alisisitiza.

Jaji Ramadhani alishauri ni vizuri kila mjumbe wa bunge hilo akaacha mapenzi kwa vyama vyao na kila kitu na kutanguliza maslahi ya taifa kama wajumbe wa tume  ya kuratibu maoni ya katiba  walivyofanya  na kuwezesha kuandaa rasimu mbili.

Alisema ni ukweli usiopingika kuwa mabadiliko kwa sasa ni  lazima, sababu kila wakati na mambo yake na sasa miaka 50 imepita na hivyo kuna umuhimu wa kupata kitabu kingine cha katiba itakayokwenda na wakati.

Rais wa TLS, Francis  Stolla, alisihi wajumbe hao kuongozwa na maoni ya Watanzania  na kufahamu vizuri kifungu cha 25 cha sheria hiyo,  lakini  akidai hajakielewa vizuri kwa sababu hakijafafanua kikamilifu  madaraka ya bunge hilo.

Alisema ni vema wakaelewa mwisho wa siku katiba hiyo ikipitishwa na  bunge hilo  itarudi kwa wananchi ili  kuipigia kura, hivyo kama mawazo ya wananchi yameachwa kwa vyovyote wataikataa katiba hiyo.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...