Monday 23 February 2015

TUSEME BASI KWA MAUAJI YA ALBINO

TUSEME BASI KWA MAUAJI YA ALBINO!
   


Ninashindwa kuelewa nianzie wapi kuandika hii makala ya leo.Maana ninaandika mikono ikitetemeka kwa kweli. Nashindwa kuelewa hasa lawama zangu nizielekeze kwa nani. Sijui kama ni kwa serikali au wananchi,ama kwa wote.
Hivi ni kweli tumeshindwa kuwalinda watu wenye ulemavu wa ngozi? Hawa watu wenye ulemavu wa ngozi wanaishi wapi na wanao waua kikatili nao wanaishi wapi? Je,wanaishi katika nchi tofauti au sayari tofauti? Kama la, je ni kweli jamii inayoishi katika maeneo husika haijui ni nani wanaotenda vitendo hivyo? Kama wanajua kwanini wanakaa kimya?

Je, ni kweli serikali ya Tanzania imeshindwa kabisa kukomesha ukatili huu? Je,tuchukue sheria mikononi na tuanze kuwateketeza waganga wa kienyeji wote wanaoishi katika maeneo husika?Nadhani hii ndiyo njia pekee maana bila ya wao haya yasingetokea. Kama serikali yetu imeshindwa kuwalinda watu wenye ulemavu wa ngozi wananchi tuchukue jukumu hili. Wananchi wa maeneo husika kuweni sungusungu katika kaya zenu na hususan kama kuna familia zenye watu wa ulemavu wa ngozi. Watoto hawa kama vile zinavyojengwa maabara basi zijengwe shule maalum kwaajili yao na ziwe mbali na maeneo hayo wanayoishi ambako yametawaliwa na hizo imani potofu.
Lakini tujiulize nini chanzo cha imani hizi kwa wananchi wa maeneo haya.Mimi Napata jibu hili, UJINGA na UMASIKINI. Wakazi wa maeneo husika wangekuwa na elimu wasingeamini ushirikina kwani hata hao wanaonunua viungo hivyo wangeshindwa pa kuanzia.
Umasikini nao unafanya mtu aweze kufanya chochote ili akabiliane na maisha. Hivi vitu viwili huenda pamoja na ni adui mbaya sana katika maendeleo.
Serikali pamoja na taasisi binafsi zisaidie katika kutoa elimu kwa jamii za maeneo haya. Hii itachukua muda mrefu ila italeta suluhisho la kudumu. Wakati mchakato wa kutoa elimu ukiendelea, serikali ikishirikiana na jamii katika maeneo husika iwasake watuhumiwa wa ukatili huu ili wafikishwe katika vyombo vya sheria.

Serikali iweke donge nono kwa wale watakaosaidia kutoa taarifa za wahalifu hawa.Mimi ni imani kuwa wanajulikana kwani wanaishi katika jamii hiyo hiyo. Wanaofanya hayo ni wanajamii wenyewe yaani  baba wa familia, watoto wa familia, jamaa wa familia, jirani wa familia n.k

 Na pale watakapothibitika,adhabu kali ichukuliwe juu yao.

         TUSEME BASI KWA MAUAJI YA ALBINO!
Imeandikwa na


Anna Nindi

No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...