Sunday 29 December 2013

Polisi yanasa meno ya tembo ya 25m/= kwenye treni


Kaimu kamanda wa kikosi cha polisi cha Tazara, (SSP) Inocent Mgaya (katikati) akiwa na OCD wa kituo hicho SP, Bakari Makuka (kushoto) na SP, Shaaban Hussein wakionesha meno ya tembo 
Meno ya tembo yenye thamani ya Sh. milioni 25.5 yamekamatwa ndani ya treni ya Tazara katika stesheni ya Kisaki, Wilaya ya Morogoro Vijijini,  yakisafirishwa kuelekea jijini Dar es Salaam.
 
Meno hayo yalikamatwa Alhamisi wiki hii, ikiwa ni siku chache baada ya mawaziri wanne kuondolewa madarakani kutokana na kutosimamia vizuri zoezi la 'Operesheni tokomeza majangili '.
 
Akizungumza jana, Kaimu kamanda wa kikosi cha polisi cha Tazara, (SSP) Inocent Mgaya, alisema katika tukio hilo alikamatwa Ally Juma (26), maarufu Ngagari, fundi seremala  na mkazi wa Kisaki.
 
Kamanda Mgaya, alisema walipata taarifa kutoka kwa raia mwema kuwa kuna mtu amebeba meno ya tembo ndani ya treni hiyo iliyokuwa ikitokea Zambia kwenda jijini Dar es Salaam.
 
Alisema baada ya kufanya upekuzi katika behewa namba M2, walifanikiwa kumkamata mtu huyo akiwa na mabegi mawili yakiwa yamehifadhiwa pembe 14 za tembo na kipande kimoja cha jino la kiboko.
 
"Tulipomkamata na kumfanyia upekuzi tuligundua begi la kwanza lilikuwa na vipande vinane vya pembe nane na la pili aliweka vipande saba," alisema Kamanda Mgaya.
 
Alisema kwa kushirikiana na wataalamu kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, walibaini vipande hivyo vya pembe za tembo vina uzito wa kilo 29 vyenye  thamani ya Dola za Kimarekani 1950 (Sh. 25,520,000).
 
Jino la kiboko lilikutwa na uzito wa gramu 900 lenye thamani ya Sh. milioni 2.5.
 
"Nataka kuweka wazi kwamba usafiri wa treni ni kwa ajili ya watu kupata usafiri wa uhakika na sio vinginevyo, polisi wapo  makini kuhakikisha hakuna mtu anayetumia chombo hiki kwa uhalifu," alisema.
 
Aidha, kwenye tukio hilo polisi walikamata mifuko miwili ikiwa imepakiwa madawa ya kulevya aina ya bangi.
 
Hata hivyo, hakuna mtu aliyekamatwa kuhisika na mifuko hiyo yenye uzito wa kilo 19.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...