Wednesday 1 April 2015

TEMBEA UONE: ADHA YA USAFIRI KISIWANI MAFIA



Ni majira ya saa 2 usiku,tupo nje ya hoteli tuliyofikia kisiwani Mafia,tunaona watu wengi wakipita na mizigo kichwani na mikononi kuelekea upande mwingine. Tunauliza wenyeji wetu ni wapi walikuwa wakielekea watu wale. Walitujibu kuwa walikuwa wakielekea bandarini kupanda “chombo” kuelekea Dar es salaam. Nilidadisi zaidi kutaka kujua hicho “chombo” kilikuwa ni nini? Nijibiwa kuwa kilikuwa ni “jahazi”. Niligundua kuwa usafiri wa Mafia kwenda Dar haukuwa ni wa kila siku.


Nilipatwa na udadisi zaidi wa kutaka kwenda kuona mandhari ya “bandari na chombo” chenyewe mara nitakapopata nafasi.Baada ya siku kadhaa kulikuwa na usafiri tena. Majira ya saa 2 usiku tukifuatana na mwenyeji wetu,tukaenda kuona mandhari ya bandari na chombo.
Nilipigwa na butwaa tulivyofika pale kwani kuna mambo ambayo kwangu hayakukaa sawa.Kwanza, palikuwa giza na sikuweza kuona chochote. Pili,nilidhani ni bandari kama bandari nyingine tulizozoea,yaani kuona vyombo ya usafiri vikiwa vimeegesha.Pale hatukuona kitu. 
Kilichotushangaza zaidi ni kuona watu, wakiwa na mizigo yao, wakielekea baharini. Tulisogea karibu ili kuelewa nini kilikuwa kinaendelea. Watu walikuwa wakiingia katika boti ndogo wakiwa na mizigo yao. Boti hiyo ndiyo ilitumika kuwapeleka watu kwenye jahazi ambalo lilikuwa kwenye maji mengi na halikuonekana katika upeo wa macho yetu. Jahazi hilo ndilo lingewapeleka Dar es salaam kupitia Kisiju, Pwani, ambapo ndipo wangeshukia.
Kisiju Mkuranga Pwani
Haya ndiyo majahazi ya kwenda Mafia,Kisiju, Mkuranga,  Pwani. (PICHA kwa hisani ya tulonge.com)


Nilibaki mdomo wazi na woga ukiwa umenijaa.Kwani niliona kabisa kuwa safari ya watu wale ilikuwa ni safari isiyo na uhakika. Niliwafikiria zaidi kina mama na watoto ambao walikuwemo katika safari ile. Hivi ni kweli, watanzania hawa wanashindwa kupatiwa usafiri wa uhakika?
Usafiri wa ndege ulikuwepo kwa ndege ndogo za Coastal Aviation.Ndege inayochukua abiria 12 tu au chini ya hapo. Na hata hivyo ndege ni gharama kwa wakazi wa Mafia ambao wengi ni wavuvi na wakulima ambao kipato chao ni kidogo. Sijui kwa wale wa Mafia kama hali hii imebadilika.

KWELI TEMBEA UONE.

Imeandikwa na Anna Nindi


No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...