Thursday 12 September 2013

NI KWELI WATANZANIA HAWANA UWEZO WA KUNISAIDIA ILI NISIFE


Inauma sana unapoona familia ndio inakutegemea, halafu unayetegemewa mwenyewe unaumwa kama hivi.Mbaya zaidi kadri ninavyohangaika ili kupona, hali ndio inazidi kuwa mbaya zaidi. Nimekuwa nikitokwa na usaa mwingi mno, kwa dakika tu hata kikombe kinajaa, nilikwenda hospitali wamezuia hilo.Sasa uvimbe naona unakua, maumivu ninayoyapata ni makali mno.Naombeani mniokoe nipate fedha nikatibiwe.(Kama umeguswa kumsaidia unaweza kupiga namba 0754498972)
Joseph Ayubu ni mkazi wa Kijiji cha  Nyenze, Shinyanga.Ugonjwa unaomsumbua  unaendelea kumwathiri, huku akiwa hana uwezo wa matibabu.
Maisha yamejaa changamoto, unaweza kulia kwa sababu ya tatizo hili, mwingine akalia kwa lile.
Wataalamu wa saikolojia, wakiwemo  Fernald LD na Hockenbury Hockenbury kutoka New Zealand,  wanasisitiza katika machapisho yao kadhaa yakiwemo kitabu cha Life is like this, yaani maisha ni kama hivi, kwamba unapokuwa na tatizo, tuliza kichwa, tafakari sababu hasa ni nini na nini cha kufanya ili kuondokana na hali hiyo.
Ilimradi uko hai, shida zipo, huna sababu ya kukata tamaa, cha msingi chukua hatua kuzishinda shida zinazokusumbua, ikiwezekana shirikisha wengine.

Mfano wa Joseph Ayubu
Joseph Ayubu (40) mkazi wa Kijiji cha  Nyenze wilayani Kishapu,  mkoani Shinyanga, kwa miaka mingi amekuwa akihangaika kupata tiba ya tatizo lake bila mafanikio.
Ayubu anateswa na ugonjwa wa kansa, hali yake kwa sasa ni mbaya, anatokwa na usaa mwingi; akiukinga usaha unaotoka shingoni, kikombe hujaa ndani ya dakika moja.
“Nimevumilia mno, kadri siku zinavyokwenda mbele naona kifo kinakuja. Sitaki kuamini kama ulimwengu wote au Watanzania wote wanaweza kuwa na roho ngumu ya kushindwa kuniokoa, naomba msaada niondokane na shida hii,”  anasema Ayubu.
 Anawaomba wasamaria wema wamchangie fedha  ili akatibiwe katika Hospitali ya KCMC iliyoko mkoani Kilimanjaro.
Ayubu anasumbuliwa na tatizo la saratani  ya shingo, hivyo kusababisha shingo yake kuvimba na kumfanya ashindwe kutoa sauti  ipasavyo kwani sehemu kubwa ya koo lake imeziba.
Anaeleza kuwa kutokana na ugonjwa huo, kichwa nacho kinazidi kuvimba na kupata maumivu makali.
Macho nayo yanavimba na kumsababishia ashindwe kuona  mbali. Mbaya zaidi ni kwamba kwa namna anavyoona, kila siku ugonjwa unaendelea kukua katika mwili wake.
Anasema ugonjwa huo umeshindikana kutibiwa katika hospitali za kawaida hivyo anatakiwa aende kutibiwa Hospitali ya KCMC (Kilimanjaro Christian Medical Centre).
Ayubu anatakiwa  kuchomwa sindano sita, kila sindano gharama yake Sh218,000, hivyo anatakiwa awe na  Sh1,308,000 kwa matibabu hayo pekee, nje ya tiba zingine, gharama za kuishi huko KCMC na mengineyo.
Ugonjwa ulivyoanza
Alianza kuugua maradhi hayo mwaka 2010,  ulianza uvimbe mdogo shingoni, baadaye ukaongezeka, ikamlazimu kununua dawa za kutuliza maumivu hasa Panadol, kwa vile uvimbe huo ulikuwa unasababisha maumivu makali.
“Hali yangu ya kiafya inazidi kudhoofika, siwezi tena kufanya kazi za kuniingizia kipato kwani maumivu ninayoyahisi ni Mungu tu ndio anajua, ni maumivu makali mno. Ninaomba sana Watanzania wenzangu na yeyote ambaye si Mtanzania anisaidie, nina mke na watoto ambao bado wadogo na sina namna ya kuwasaidia kwa sasa”anasema.
“Wakati mwingine mwili wangu unakufa ganzi na fahamu kupotea, wakati mwingine fahamu zinarudi naweza kujielewa vizuri, ninachokisubiri kwa sasa ni huruma yenu Watanzania, ndiyo itasababisha maisha yangu kurudi kama nilivyokuwa mwanzo”
Anasema watoto wake wanasoma lakini kwa sasa wamesimamishwa kwa sababu hana fedha za kuwalipia ada na huduma zingine za masomo.
Anasema alipokuwa hajaugua ugonjwa huo alikuwa akifanya shughuli mbalimbali ndogo ndogo za kuingiza kipato, huku akifanya pia kazi kama Mwalimu wa Kwaya katika Kanisa la KKKT kijijini hapo. Kwa sasa hawezi tena kufanya kazi yoyote kwa sababu ya maumivu makali anayohisi na pia hali ngumu ya kiafya inayoendelea kumsumbua.
“Nimeshawahi kwenda hospitali mbalimbali mkoani hapa lakini hali haibadiliki, nilienda hadi kwa waganga wa kienyeji, ugonjwa unaongezeka.
Hali yake kwa sasa ni mbaya, ndani ya dakika moja naweza kujaza usaha kwenye kikombe, huku maumivu yakiendelea kuwa makali zaidi.
Ayubu anasema ameendelea hivyo, mpaka alipokwenda Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga, ambako alishonwa ndipo angalau sasa usaha umepungua, ingawa hali yake bado ni mbaya hasa shingo kuendelea kuvimba.
“Mpaka sasa siwezi kugeuka nikitaka kugeuka inabidi nigeuze mwili wote sio siri nateseka sana endapo maumivu haya yangekuwa yanawezekana kumwachia mtu mwingine ningekupa ukaona maumivu yake.
“Nina watoto wananitegemea, nilikuwa nalima na kufanya biashara mbalimbali, kwa sasa siwezi kutokana na kupata maumivu makali ambayo yananisababishia hata kushindwa kula”anasema Ayubu.
Maisha yake kwa sasa yamekuwa ya kubahatisha, kuna wakati hulala bila kula japo ni mgonjwa.
“Sisi Watanzania wote ni ndugu nihurumieni mwenzenu naumia, naomba sana mnisaidie kulingana na ulichonacho,”anasema Ayubu huku akitokwa  machozi.
Kwa mujibu wa Ayubu, madaktari wamemshauri kwamba akipata fedha hizo tatizo lake linaweza kutibiwa na kurudi katika hali yake ya kawaida.
Kwa mujibu wa vitabu vitakatifu, kusaidia wenye uhitaji huchangia kupata baraka katika maisha, lakini kama wanadamu tunapaswa kusaidiana...duniani tunapita.
Kwa yeyote mwenye moyo wa kumsaidia chochote, Ayubu awasiliane na Mhariri wa Jarida la Ndani ya Habari, 0754498972.

No comments:

Post a Comment

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...