Showing posts with label MADA YA SIKU. Show all posts
Showing posts with label MADA YA SIKU. Show all posts

Wednesday, 2 December 2015

KILA KIUMBE WA KIKE- CHRIS MAUKI


Wanaume wenzangu tuelewe na pia hili lituingie akilini kwamba sisi na wake zetu tumeumbwa tofauti sana. Kila mwanamke ndani ya moyo wake na nafsi yake kuna kiu isiyo na msimu. Kiu iliayo kwa sauti ikitamani kudekezwa, kupendwa, kujaliwa na kuangaliwa kwa upendo kama mtoto mdogo. Sasa wewe leo mwenzako anadeka kidogo unamkurupusha kama mwizi eti "acha utoto weweee, unamdekea nani sasa" nani kakwambia mapenzi yana kukua, au yana ukubwa na udogo? Usiishi na mke wako kama mwanaume mwenzako, usimfanye yeye kama kifaa, yeye sio trekta au jiko au kompyuta au sufuria. Yeye ni kiumbe mwenye hisia tena kali tofauti kabisa na wewe. Kama haujafundishwa basi kamuulize mama yako atakwambia, na kama atakwambia tofauti basi mlaumu baba yako kwa kumfanya mama yako akawa kama wewe unavyomfanya mke wako leo. Pokea hiyo kwa leo - Chris Mauki

Friday, 2 October 2015

MOTHER AND DAUGHTER LOVE!

Katika safari ya maisha mtu ambaye hawezi kukukana na atakayekuwa na wewe siku zote,katika shida na raha ni MAMA YAKO TU.
Kwa mama anaejitambua,mtoto wake ndiyo kila kitu kwake.
Siku zote mama humtakia mwanae mafanikio na huumizwa na tatizo litakalompata mwanae.Mama ndiye pekee  anayeweza kukusikiliza na kuamini unachosema.Mama ndiye anajua tabia halisi ya mwanae.Mama anajua udhaifu na ushupavu wa mwanae.
Mama ndiye unayeweza kumweleza matatizo yako akakusikiliza na kukusaidia kwa uwezo wake.Kwanini?Kwa sababu unapoumia wewe na yeye huumia pia.
Baba anaweza kumwacha mama yako na akaenda kutafuta mwanamke mwingine.Ila mama wengi ni wagumu kuwacha watoto wao walelewe na watu wengine.Kwanini?Kwa kuhofia kuwa mama wa kambo au mtu mwingine hataweza kumpa mtoto wake mapenzi halisi ya mama.Ingawa si mama wa kambo wote ambao wana roho mbaya.
Tuwaheshimu mama wote wanaojitambua.
NANI KAMA MAMA.

Monday, 23 February 2015

TUSEME BASI KWA MAUAJI YA ALBINO

TUSEME BASI KWA MAUAJI YA ALBINO!
   


Ninashindwa kuelewa nianzie wapi kuandika hii makala ya leo.Maana ninaandika mikono ikitetemeka kwa kweli. Nashindwa kuelewa hasa lawama zangu nizielekeze kwa nani. Sijui kama ni kwa serikali au wananchi,ama kwa wote.
Hivi ni kweli tumeshindwa kuwalinda watu wenye ulemavu wa ngozi? Hawa watu wenye ulemavu wa ngozi wanaishi wapi na wanao waua kikatili nao wanaishi wapi? Je,wanaishi katika nchi tofauti au sayari tofauti? Kama la, je ni kweli jamii inayoishi katika maeneo husika haijui ni nani wanaotenda vitendo hivyo? Kama wanajua kwanini wanakaa kimya?

Friday, 13 February 2015

MADA YA SIKU: JE, KUNA UMUHIMU WA KUWA NA PF3?

Nimekuwa nikitatizika sana na swala la PF3,nadhani wengi tunajua kuwa ni kitu gani. Hivi ni haki kukimbilia polisi kuchukua PF3 kwanza badala ya kumkimbiza majeruhi hospitali?Hii imekaaje wadau.

Majeruhi wengi ambao wamepoteza maisha wangeweza kuokolewa kwa wakati kama si kukimbilia PF3 kwanza katika vituo vya polisi badala ya kukimbilia hospitali kwanza. Hata waliopewa sumu n.k wanaweza kuokolewa katika muda mwafaka.

Siwezi kusema moja kwa moja kama wazo la kuwa na PF3 halifai sababu sijui walioweka walikuwa na makusudi gani bali ninaweza kutoa mawazo yangu katika hili.Nadhani ingekuwa vyema polisi wakaweka dawati lao katika hospitali zote muhimu na kutoa hizo PF3 sambamba na majeruhi kuhudumiwa ili kuokoa maisha ya majeruhi.

Kwa mfano majeruhi anayetokwa na damu kwa wingi anaweza kusaidiwa kuzuia utokaji wa damu hiyo na hapohapo kupewa damu nyingine na hivyo kuokoa maisha yake.Huwezi kuokoa maisha ya majeruhi huyu kwa kukimbilia kituo cha polisi kwanza kuchukua PF3!.



Je, wewe mdau una mawazo gani?

Wednesday, 11 February 2015

MADA YA SIKU: NI HALALI MTU KUGONGWA KATIKA ALAMA YA PUNDAMILIA?

Pundamilia ni moja katika alama za barabarani.Alama hii ina maana ni sehemu ya kuvuka waenda kwa miguu na magari hutakiwa kusimama.Nimekuwa nikishangazwa mara kwa mara kusoma kuhusu watu kugongwa na magari katika alama hizi.Nimeshuhudia mwenyewe vilevile jinsi madereva wanavyokaidi kusimama katika alama hizi.Madereva wanapita kama vile hakuna alama yeyote.Hii inasikitisha sana.Maana inaleta maana kuwa barabara ni haki ya waendesha vyombo vya moto na si kwa watembea miguu. Sweden,alama za barabarani zinaheshimika mno.Madereva wanazingatia sana mwendokasi ulioweka mfano katika eneo la shule ambapo magari hutakiwa kutembea  si zaidi ya  kilomita 30 kwa saa. Kwenye alama ya pundamilia,hata kama wewe mvuka kwa miguu utaona gari inakuja  na kuwa na shaka kuwa dereva atapita,huwa haiwi hivyo.Dereva atasimama na kukuonyesha ishara ya kuvuka! Sweden, kosa la dereva kuzembea katika alama za barabarani hupelekea dereva huyo kufungwa jela na kupoteza leseni. Na hata ukitaka kupata leseni tena baada ya kutumikia adhabu inabidi ufuate taratibu upya kama mtu asiyekuwa na leseni.Taratibu zenyewe zina mlolongo mrefu na ni gharama.

Inasikitisha nchini kwetu kuona watoto wa shule wanagongwa na kufa tena nje ya shule zao.Hivi hawa wanaogonga watoto na raia wengine katika alama za pundamilia huchukuliwa hatua gani?Au ndiyo marehemu hana haki?

Nadhani imefikia wakati wa kubadilishwa kwa sheria za barabarani zisizokidhi nchini Tanzania.Nina imani sheria  ngumu zitapunguza sana ajali za barabarani.


Je,sheria zetu zikoje?

Saturday, 13 September 2014

MADA YA SIKU: URAIA PACHA

Swala la uraia pacha limetawala bunge maalumu la katiba. Wajumbe mbalimbali wa bunge hilo  wamekuwa wakitoa mawazo yao kuhusu uraia pacha.Wako wanaoona kuwa uraia pacha hauna madhara na wapo wanaopingana na dhana hiyo.
Kwa upande wangu sioni tatizo lolote kwani Tanzania itakuwa si nchi ya kwanza kuwa na uraia pacha.Kuna chini nyingi tu duniani, zikiwemo zile za Afrika ambazo zimeruhusu uraia pacha na hatujaona tatizo lolote.
Baadhi ya nchi za Afrika ambazo zinaruhusu uraia pacha ni Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Namibia,Nigeria, Lesotho, Sierra Leone, Togo,Afrika ya Kusini (kwa kibali maalum kutoka wizara ya mambo ya nje), Ghana(raia mwenye uraia pacha haruhusiwi kushika nafasi za juu za uongozi)n.k.
Kutokana na mageuzi yanayoendelea duniani sisi kama nchi, hatuwezi kujitenga na mabadiliko haya.Vinginevyo wakati wenzetu wanakimbia,sisi tutakuwa tunatembea.
Kama kuna wasiwasi juu ya uraia pacha tunaweza kuweka vipengele ambavyo vitasaidia kuzuia vitu vinavyoonekana ni hatari mfano kama walivyofanya Ghana kuzuia mtu mwenye urai pacha kushika nafasi za juu za uongozi. Wanaweza vilevile kubana umiliki wa ardhi kwa mtu mwenye uraia pacha ambaye si mzawa n.k
Je kwako wewe msomaji uraia pacha ni hatari kwa taifa?Kama ndivyo hatari hizo ni zipi?Toa mawazo yako na tutayaweka hapa.

PALM TREES ARE BEAUTIFUL

Minazi huleta mandhari nzuri ya kuvutia, haijalishi ni sehemu gani imemea. Palm trees are always beautiful, it doesn´t matter where they are...